Tuesday, May 22, 2012

ABIDAL ARUHUSIWA KUTOKA HOSPITALI.



KLABU ya Barcelona imesema kuwa beki wake Eric Abidal ameruhusiwa kutoka hospitali jana ikiwa ni wiki sita toka alipofanyiwa upasuaji wa kupandikiza ini jingine. Katika taarifa iliyotolewa na klabu hiyo mchezaji huyo atakuwa akihudhuria kliniki mara kwa mara kwa ajili ya kuangalia maendeleo yake kiafya kutokana na upasuaji huo aliofanyiwa. Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ufaransa mwenye umri wa miaka 32 alifanyiwa upasuaji wa kupandikizwa ini ambalo alipewa na mpwa wake April 10 mwaka huu. Abidal aliwahi kufanyiwa upasuaji kuondoa uvimbe uliokuwa umeota katika ini lake Machi mwaka jana na baadae kurejea uwanjani lakini alirudishwa tena hospitali baada ya madaktari kugundua kuwa ilikuwa ni lazima afanyiwe upasuaji wa kupandikiza ini jingine. Klabu yake ya Barcelona ambayo haijabeba kombe lolote msimu huu imebakiwa na mchezo mmoja wa fainali ya Kombe la Mfalme dhidi ya timu ya Athletic Bilbao mchezo ambao utachezwa katika Uwanja wa Calderon jijini Madrid, Hispania.

No comments:

Post a Comment