Thursday, May 17, 2012

TAARIFA MBALIMBALI KUTOKA TFF LEO.

RAMBIRAMBI MSIBA WA PATRICK MAFISANGO
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha mchezaji wa Simba na timu ya Taifa ya Rwanda (Amavubi), Patrick Mafisango kilichotokea leo alfajiri (Mei 17 mwaka huu) kwa ajali ya gari Dar es Salaam.
Msiba huo ni mkubwa kwa familia ya mpira wa miguu kwani Mafisango kwa kipindi chote alichocheza mpira hapa nchini akiwa na timu za Azam na baadaye Simba, aliifanya kazi yake (kucheza mpira) kwa bidii. Kifo chake ni pigo kubwa si tu kwa familia yake na timu alizochezea, bali ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati ambapo changamoto zake zilikuwa dhahiri uwanjani.
Wakati mauti inamkuta, Mafisango alikuwa ameitwa Amavubi kwa ajili ya mechi za mchujo za Kombe la Dunia, Kanda ya Afrika zinazochezwa mapema mwezi ujao. TFF inatoa pole kwa familia ya Mafisango, klabu ya Simba, Shirikisho la Mpira wa Miguu Rwanda (FERWAFA) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito. Mungu aiweke roho ya marehemu Mafisango mahali pema peponi. Amina

1,000/- TU KUONA TWIGA STARS, BANYANA BANYANA
Kiingilio kwenye mechi ya kirafiki ya kimataifa kati ya timu ya Taifa ya wanawake (Twiga Stars) na Afrika Kusini (Banyana Banyana) itakayochezwa Jumalipi (Mei 20 mwaka huu) ni sh. 1,000. Mechi hiyo ambayo ni sehemu ya maandalizi kwa timu hizo zinazoshiriki mashindano ya Afrika itafanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10.30 jioni. Viingilio hivyo ni kwa maeneo yote, isipokuwa VIP A ambapo itakuwa sh. 10,000 na VIP B sh. 5,000. Baada ya mechi hiyo, Twiga Stars itakwenda Ethiopia kwa ajili ya mechi ya mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) itakayochezwa Mei 27 mwaka huu jijini Addis Ababa. Tayari Meneja Usalama wa Chama cha Mpira wa Miguu Afrika Kusini (SAFA), Percy Makhanya ameshawasili nchini kuratibu ujio wa Banyana Banyana. Timu hiyo pia iko katika kinyang’anyiro cha kutafuta tiketi ya Fainali za Nane za AWC ambapo katika raundi hii ya pili imepangiwa Zambia na itaanzia mechi hiyo ugenini jijini Lusaka.

No comments:

Post a Comment