Thursday, April 5, 2012

MOURINHO AIGWAYA BAYERN.

MENEJA wa Real Madrid Jose Mourinho amependekeza kuwa hategemei kukutana na klabu yake ya zamani Chelsea katika fainali ya michuano ya Kombe la Klabu Bingwa Ulaya. Madrid katika mchezo wa nusu fainali ya michuano hiyo itakutana na Bayern Munich baada ya kufanikiwa kuifunga APOEL Nicosia, wakati Chelsea wenyewe watakutana na Barcelona. Lakini Mourinho ambaye amekuwa akilalamika kuwa waamuzi wamekuwa wakiipendelea Barcelona haamini kwamba kikosi chake kitakutana na Chelsea katika mchezo wa fainali akidai kwamba fainali itakuwa kati ya Bayern na Barcelona. Madrid wamefanikiwa kuwafunga mahasimu wao Barcelona mara moja katika michezo 10 waliyokutana toka Mourinho aanze kuinoa klabu hiyo akitokea Inter Milan mwaka 2010. Mourinho amesema huwa jambo ambalo haliwezekani timu kuishinda Barcelona katika Uwanja wa Camp Nou kwa uzoefu wake toka alipokuwa akikinoa kikosi cha Chelsea huko nyuma, lakini pia akasema kuwa wapinzani wao katika nusu fainali Bayern nayo ni timu ngumu ingawa anaifahamu vizuri kwakuwa haijabadilika toka alipokuwa katika kipindi cha miaka miwili.

No comments:

Post a Comment