Wednesday, May 16, 2012

TETESI ZA USAJILI: MWAPE, ASAMOAH, BABU NJE YANGA.

Shadrack Nsajigwa
KLABU ya Yanga imewatema rasmi katika usajili wake, washambuliaji Davies Mwape kutoka Zambia na Kenneth Asamoah wa Ghana, wakati Nahodha Nsajigwa Shadrack 'Fusso' anaweza kutolewa kwa mkopo sawa na Abuu Ubwa na Bakari Mbega. Habari kutoka Kamati ya Ufundi ya Yanga, iliyo chini ya Mwenyekiti wake, Mohamed Bhinda ni kwamba benchi la ufundi limependekeza wachezaji hao waachwe kwa sababu hawana msaada kwenye timu. “Ambao mikataba yao imeisha tunawaacha moja kwa moja, ambao bado wana mikataba itabidi tuwatoe kwa mkopo,”kilisema chanzo kutoka Kamati ya Ufundi. Aidha, chanzo kimesema kwamba msimu huu, Yanga itaelekeza nguvu zake kwenye kikosi cha pili zaidi- kuhakikisha wanawekeza zaidi huko ili kuvuna wachezaji bora. “Tutasajili timu imara ya kikosi cha kwanza kwa ajili ya msimu ujao wa ligi, lakini pia tutahakikisha tunawkeza sana kwenye timu B,”kilisema chanzo hicho. Wakati Nsajigwa alikuwa uchochoro Mei 6, mwaka huu Yanga ikifungwa 5-0 na SImba, Asamoah na Mwape wameshindwa kuifungia mabao ya kutosha timu hiyo katika Ligi Kuu. 

STORY BIN ZUBERI

No comments:

Post a Comment