Thursday, May 24, 2012

KASEJA NAHODHA MPYA STARS.

Juma K. Juma.
NDOTO za mlinda mlango namba moja Tanzania, Juma Kaseja kuwa Nahodha wa timu ya taifa, zimetimia baada ya benchi la ufundi la Taifa Stars, kumteua kipa huyo wa Simba SC kushika wadhifa huo. Maofisa wa benchi la ufundi la Stars, chini ya kocha Kim Poulsen, Wasaidizi wake, Sylvester Marsh na Juma Pondamali kwa pamoja na Meneja Leopold Mukebezi, baada ya kikao chao wamemteua rasmi Kaseja kuwa Nahodha wa timu hiyo, akirithi mikoba ya beki wa kulia, Nsajigwa Shadrack ambaye ameachwa kwenye kikosi hicho. Hata hivyo, haijafahamika kama Kaseja atakuwa Nahodha wa kudumu wau muda wa Stars, kwa sababu chini ya Jan Poulsen, aliyekuwa kocha wa Taifa Stars kabla ya Kim, Shaaban Nditi ndiye aliyekuwa anapewa mikoba ya Unahodha Nsajigwa anapokuwa nje ya kikosi. Hata mbele ya wachezaji wenzao, Nditi anakubalika zaidi kuliko Kaseja ambaye pia ni Nahodha wa Simba na wengi wanaamini uteuzi huo ungeshirikisha wachezaji- basi hiyo ingekuwa nafasi ya kiungo mkabaji wa Mtibwa Sugar ya Morogoro. “Kama tungepiga kura za siri, mimi nakuambia Nditi angekuwa Nahodha, ila hata Kaseja kwetu si tatizo, timu ina umoja na tutampa ushirikiano,”alisema kiungo mmoja wa Stars, ambaye hakupenda kutajwa jina lake.

SOURCE: BIN ZUBERY

No comments:

Post a Comment